Thursday, March 5, 2009

Michael Uledi katutoka....

Mwandishi wa habari wa Magazeti ya Mwananchi katika kituo cha Dodoma Michael Uledi amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika hospitali ya Mirembe alipokuwa amelazwa baada ya kuugua kwa muda mrefu.

Marehemu Uledi ambaye ameugua TB kwa muda mrefu alizaliwa mnamo mwaka 1969 katika Kijiji cha Buigiri wilaya ya Chamwino.

Marehemu ambaye ameacha Mke na mtoto mmoja atazikwa kesho Ijumaa kijijini kwao Buigiri.

Marehemu Uledi alisoma katika shule ya msingi Buigiri 1977-1983 na baadae mwaka 1986 alijiunga katika shule ya Sekondari ya Chidya wilaya ya Masasi ambako alimaliza kidato cha nne mwaka 1989.


Taarifa za kifo cha Uledi zilitolewa jana na Mke wa marehemu Agness Mzola baada ya kufika hospitalini na kuambiwa kuwa Maiko alikuwa amefariki dunia na ndipo alipoanza kutoa taarifa kwa ndugu na wahusika wa karibu na marehemu.

Mwaka 1990 alijiunga na shule ya sekondari ya Moshi kwa ajili ya masomo ya kidato cha tano na sita ambako alimaliza mwaka 1992 na baadae alijunga katika mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa mkoani Mara ambako alihitimu na kasha alikwenda Jijini Dar Es Salaamu ambako alifanya kazi katika makampuni ya watu binafsi kwa kipindi cha miaka miwili.

Uledi alijiunga na MAMET kwa ajili ya kozi ya Uandishi wa Habari kwa muda wa miezi mitatu na alipomaliza alijiunga na shirika la IPP mwaka 1998 ambapo alipangiwa kituo cha Dodoma akiwa ni Mwandishi wa magazeti ya Nipashe na Gadiani pamoja na Radio One.

Alijiunga na chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini kilichopo mjini Dodoma mwaka 2001 hadi 2003 ambapo alimaliza Shahada ya juu ya Mipango na Maendeleo Vijijini na kufanya kazi kwa muda mfupi katika shirika la Viwanda Vidogo mkoani Dodoma (SIDO) na baadae alihamishiwa katika kituo cha kazi Mtwara.

Mwaka 2004 hadi 2006 alifanya kazi katika Benki ya Exims katika wilaya ya Masasi akiwa ni Meneja Msaidizi wa Bank na baadae alikaa mkoani Morogoro kwa muda mfupi ambako alikuwa akiandika katika gazeti la serikali la Habari Leo.

Januari mwaka 2007 alijiunga na kampuni ya Mwananchi Communications ambao ni wachapishaji wa magazeti ya Mwananchi,Citizen na Mwanasport kazi aliyoifanya hadi mauti yanamchukua.

Alikuwa ni mjumbe katika umoja wa waandishi wa habari za Bunge ambae alikuwa akiwakilisha mkoa wa Dodoma umoja ulioundwa mwaka jana.

Uledi ameacha mke na mtoto mmoja na taratibu za mazishi zinafanyika kwa kushirikiana kati ya kampuni la Mwananchi na ndugu wa marehemu nyumbani kwa Marehemu Nkuhungu mjini Dodoma, mwili wa marehemu unatarajia kusafirishwa leo kwenda Kijijii kwao Buigiri Kilomita 35 kutoka Dodoma mjini ambako mazishi yatafanyika leo saa 5 asubuhi.