Thursday, March 12, 2009

Mbunge wa Busanda afariki dunia

Mbunge wa Busanda kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi, Kabuzi Faustine Rwilomba amefariki dunia nchini India alikokuwa akitibiwa.

Kwa mujibu wa tovuti ya Bunge, Marehemu Rwilomba alizaliwa tarehe 15 Mwezi Juni 1952 na kupata elimu ya msingi katika shule za msingi Kabugozo 1964-1968 na baadaye Chewamba 1968- 1970.

Marehemu Rwilomba alipata elimu ya sekondari katika shule ya Nsumba 1971-1974 na baadaye kujiunga na chuo cha ualimu cha Korongwe ambapo alipata mafunzo ya daraja la IIIA mwaka 1975 -1976 na kutunukiwa cheti.

Alijunga na Chuo cha Ualimu Butimba mwaka 1981-1983 ambapo alipata Stashahada ya ualimu ya Sanaa (Diploma in Arts) na baadaye Chuo cha Ualimu Morogoro mwaka 1983 -1985 na kupata stashahada ya Elimu (Diploma in Education).

Mwaka 1987-1991 alijiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kupata Shahada ya kwanza ya Ualimu (B.A in Education) kabla ya kuendelea chuoni hapo na kupata Shahada ya juu ya Uzamiri ya Elimu (M.A in Education) mwaka 1993-1995.

Marehemu Rwilomba alianza kazi kama mwalimu daraja la IIIA katika shule ya msingi Hamuyembe mwaka 1975-1981, kabla ya kujiunga na Shule ya Sekondari Nsumba mwaka 1981-1984 akifundisha.

Mwaka 1985-1987 alifundisha katika Chuo cha Ualimu cha Ndala na baadaye kujiunga na Chuo cha Ualimu cha Butimba mwaka 1991-1992 akiwa Mshauri wa Wanafunzi. Mnamo mwaka 1992-1995 alijuinga na Chuo cha Ualimu Tarime kama Makamu Mkuu wa Chuo na baadaye kuwa Mkuu wa Chuo hicho mwaka 1995-2000.

Aliingia katika ulingo wa siasa mwaka 2000 ambapo alichaguliwa kuwa mbunge hadi mwaka 2005 na kisha mwaka 2005 hadi mauti yalipomkuta.

Globu hii inawapa pole wanafamilia, wanabusanda wote, wabunge pamoja na wanandugu jamaa na marafiki.

Mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi… Amen.

No comments: